Jumatatu , 15th Oct , 2018

Katika kipindi cha kuanzia septemba 20 hadi oktoba 14 mwaka huu zimekuwa siku  za majonzi na chungu kwa baadhi ya Marais wanaounda Jumuiya ya Afrika Mashariki akiwemo Rais wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli, Rais wa Kenya Uhuru Kenyata, pamoja na Rais wa Uganda Yoweri Museveni.

Rais Magufuli (kushoto), Rais Kenyatta (katikati) na Rais Museveni (kulia)

Katika kipindi hicho cha wiki 3, tumeshuhudia majonzi yakianzia kwa Rais wa Tanzania Dkt John Magufuli ambapo kulitokea ajali ya kivuko cha Mv Nyerere iliyozama katika kisiwa cha Ukara, wilayani Ukerewe huku ikishuhudiwa zaidi ya watu 200 waliokuwa wamepanda kivuko hicho wakipoteza maisha.

Mara baada ya kutokea kwa ajali hiyo viongozi wenzake kutoka Kenya, na Uganda walioneshwa kuguswa na tukio hilo na walituma salamu za rambirambi kupitia balozi zao na mitandao ya kijamii.

Oktoba 8, Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta kupitia kwa balozi wake nchini Tanzania, Dkt. Dan Kazungu alichangia shilingi Milioni 125, kwa ajili ya ajali hiyo iliyotokea Septemba 20 mwaka huu.

Oktoba 10 mwaka huu majanga yalihamia kwa nchi jirani ya Kenya kufuatia ajali ya basi katika eneo la Kericho nchini humo, ajali ambayo ilipelekea vifo vya takribani watu zaidi 50 kwa mara moja.

Kupitia tukio hilo Rais Magufuli aliandika "nimepokea kwa masikitiko taarifa ya ajali ya basi iliyotokea Kericho nchini Kenya na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 50. Nakupa pole Mhe Rais Uhuru Kenyatta, familia za marehemu na Wakenya wote. Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema na majeruhi wapone haraka".

Nimeshtushwa sana kwa familia za Wakenya wenzangu waliopoteza maisha yao katika ajali mbaya ya barabara huko Fort Ternan katika kata ya Kericho asubuhi hii na nawatakia wale walio hospitalini ahueni haraka.” aliandika Rais Kenyata

Oktoba 14 kuliripotiwa vifo vya zaidi ya watu 40  katika maporomoko ya udongo yaliyotokea wilaya ya Bududa nchini Uganda na kupelekea majonzi makubwa kwa raia wa nchi hiyo.

Rais John Magufuli alimpa pole Rais wa Uganda, Yoweri Museveni kwa kuandika, “Nakupa pole Mhe. Rais Museveni na wananchi wote wa Uganda kwa kuwapoteza watu zaidi ya 40 katika ajali ya maporomoko ya udongo iliyotokea katika wilayani Bududa. Watanzania tunaungana nanyi katika kipindi hiki cha majonzi na tunawaombea majeruhi wote wapone haraka.

Kiujumla kwa siku 25 kuanzia septemba 20 hadi oktoba 14 zimekuwa siku za majonzi na chungu kwa viongozi wa nchi hizo pamoja na raia wake kutokana na maafa yaliyotokea.

www.eatv.tv tunatoa pole kwa Rais Magufuli, Kenyata na Museveni kwa matatizo yaliyotokea kwenye nchi zao katika kipindi hicho.