Jumatano , 26th Feb , 2020

Takribani silaha 50 zimekamatwa kwenye makazi ya wakimbizi, eneo la Katumba Wilaya ya Mpanda Mkoa wa Katavi, wakati wa oparesheni iliyopewa jina la 'Safisha Katumba 2020' iliyofanywa na JWTZ kwa ajili ya kukamata silaha wanazotumia kwenye vitendo vya kihalifu na ujangili.

Mkuu wa Brigedia ya Magharibi, Brigedia Jenerali John Mkunda,

Akitoa taarifa kwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mkuu wa Brigedia ya Magharibi 202 KJ, Brigedia Jenerali John Mkunda, amesema kuwa katika oparesheni hiyo wamefanikiwa kukamata silaha takribani 50 zikiewemo SMG 13, G Three (3), Rifle (1), gobole 33 pamoja na risasi 32.

Mkuu huyo wa Brigedia ya Magharibi amesema kuwa matukio ya uhalifu yamekithiri katika Wilaya ya Katumba ambako wanaishi Watanzania wengi wenye asili ya Burundi.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Juma Homera amewataka wananchi wanaoishi katika maeneo hayo kusalimisha silaha kwa hiari yao kwani hawatosalimika wasipofanya hivyo.

"Mtakumbuka hivi karibuni Mheshimiwa Rais alipotembelea hapa alionesha kusikitika kutokana na vitendo vya kihalifu vinavyotokea katika mkoa wetu na raia hawa wa Burundi ambao waliomba uraia wa kuishi Tanzania. Kwahiyo nawaambia hakuna jiwe litasalia juu ya jiwe lingine", amesema Mkuu huyo wa Mkoa.