Jumanne , 6th Aug , 2019

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi Benjamin Kuzaga, ameeleza kutokea kwa tukio la mtoto mwenye umri wa miaka 6, aliyeuawa baada ya kuliwa na Simba, wakati akiwa amelala na mama yake katika Kijiji cha Sitalike wilayani Mpanda.

Tukio hilo limetokea mwishoni mwa wiki majira ya usiku, ambapo mtoto huyo akiwa amelala na mama yake  ndani ya nyumba ambayo haikuwa na mlango imara, walivamiwa na mnyama huyo.

"Walikuwa wanaishi nyumba ambayo haikuwa na mlango imara, huyu mtoto siku zote yuko na wazazi wake, siku ya tukio baba hakuwepo nyumbani. Ule udhaifu wa mlango ulichangia mnyama huyu kuingia ndani kirahisi," alisema Kamanda Kuzaga.

Inaelezwa mnyama huyo aliingia ndani na kumnyakua mtoto huyo na kisha kutoka naye nje, licha ya mama ake kupambania maisha na uhai wa mwanaye lakini juhudi zake hazikuzaa matunda baada ya mnyama huyo kutokomea gizani.

Baada ya polisi na wanakijiji kufika eneo la tukio, walikuta mtoto huyo tayari ameliwa na simba ambaye hawakuweza kumwona na kukuta mabaki ya kichwa na mifupa ya miguu pekee.