Alhamisi , 4th Apr , 2019

Spika Mstaafu wa Bunge la 8, Pius Msekwa amesema hatua ya Bunge kutofanya kazi na Mdhibiti na Mkaguzi Hesabu za Serikali, CAG Prof Mussa Assad ni kiashiria kwamba Bunge halina imani na CAG maana yake kiongozi huyo anapaswa kuachia ngazi.

Spika Mstaafu wa Bunge la 8, Pius Msekwa.

Spika Mstaafu Msekwa ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na kipindi cha East Africa Breakfast, cha East Africa Radio juu ya maoni yake kuhusu maazimio ya Bunge ya kutangaza kutofanya kazi na Spika.

Msekwa amesema, "Bunge likisema halitafanya kazi na kiongozi fulani, maana yake hawana imani na kiongozi fulani, ni vizuri ieleweke Bunge likisema halina imani maana yake ni kiongozi huyo tu sio idara yote, CAG akisema niachie ngazi kazi za idara yake zitaendelea na akishika mwingine kazi Bunge lisharikiana naye."

"Maafisa wa CAG wakisusia kutoingia Bungeni ni utovu wa nidhamu, kwa sababu aliyeazimiwa na Bunge ni mtu mmoja sio idara nzima, kama wakisusia kweli ni utovu wa nidhamu ni sawa na watu wakigoma kwenda kazini", ameongeza Msekwa.

April 2, 2019 jijini Dodoma, Bunge la Tanzania liliazimia kutofanya kazi na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali CAG, Prof Mussa Assad kwa kutoa kauli iliyoashiria kulidhalilisha Bunge baada ya kusema kuwa Bunge ni 'dhaifu'.