Jumanne , 14th Nov , 2017

Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na ubalozi wa Sweden zimesaini mkataba wa jumla ya shilingi bilioni 435.7 sawa na SEK bilioni 1.6 za Sweden.

Fedha hizo zimetolewa na ubalozi huo kwa serikali ya Tanzania bure ili zikatumike katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kusaidia bajeti ya serikali.

Akizungumza leo jijini Dar es salaam wakati wa kusaini mkataba huo, katibu Mkuu wa Wizara hiyo  Dotto James amebainisha kuwa katika upande wa bajeti ya serikali zaidi ya shilingi bilioni 159 sawa na SEK milioni 600 za Sweden zitaelekezwa huko kuanzia mwaka wa fedha wa 2017-2020.

Eneo jingine ambalo imeelezwa fedha hizo zitasaidia ni kuwezesha mpango wa elimu wa matokeo (EPforR) pamoja na kusaidia mpango wa kujua kusoma, kuandika na kuhesabu ambapo jumla ya kiasi cha shilingi bilioni 235 zitaelekezwa huko.

Aidha katibu huyo amesema kuwa kwa kuanza na mwaka wa fedha 2017/2018 nchi ya Sweden itatoa takribani shilingi bilioni 53.