Jumapili , 13th Sep , 2020

Mgombea Urais kupitia Chama cha Wananchi CUF Profesa Ibrahim Lipumba, amesema kuwa, endapo Watanzania watakipa chama hicho ridhaa ya kuongoza nchi kitawekeza kwenye rasilimali watu ikiwemo afya na elimu, ili kuondokana na janga la umaskini.

Mgombea Urais kupitia CUF, Profesa Ibrahim Lipumba.

Lipumba ametoa kauli hiyo hii leo Septemba 13, 2020,  wakati akizungumza kwenye mkutano wake wa kampeni mkoani Iringa, na kuongeza kuwa hali ngumu ya maisha imewafanya vijana kuonekana wazee ili hali umri wao wa kuzeeka haujafika.

"Ukiwapa CCM miaka mitano mingine hivyo vyuma si ndiyo vitatumaliza kabisa, kama hivi sasa vijana wa Ilula mnazeeka kabla ya wakati wenu unaweza ukaja hapa ukamwamkia mtu shikamoo kumbe ni kijana wa juzi bakora za CCM zimemchanganya, kila mtu yupo hoi bin taabani na ndugu zangu bakora za ccm hazina ubaguzi", amesema Profesa Lipumba

"Tunaomba kura zenu ili biashara zitoke na wananchi waweze kufanya biashara, uwekezaji uongezeke vitunguu vipate soko sio tu Tanzania mpaka Afrika Mashariki yote, watu wapewe utaalamu wa kuweza kuongeza tija katika shughuli zao za kilimo", ameongeza Profesa Lipumba.