Jumanne , 16th Apr , 2019

Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mwita Waitara amemjia juu Mbunge wa Iringa Mjini Mchungaji Petter Msigwa kwa kile alichoeleza kuwa amekuwa akijipambanua kama mtu anayepigania demokrasia lakini yeye mwenyewe kiuhalisia sio mtu wa demokrasia.

Naibu Waziri Waitara ametoa kauli hiyo Bungeni jijinin Dodoma wakati wa hitimisho wa mjadala wa bajeti wa Wizara ya TAMISEMI ambapo baadhi ya wabunge walihoji juu ya hatua ya masuala ya utawala bora.

Waitara amesema,"demokrasia inayozungumziwa kwenye nchi hii sijui ni demokrasia gani, Msigwa sijui kama yupo humu ndani, Msigwa wakati anagombea Uenyekiti wake wa Kanda walienda kuondoa Wagombea wote akabaki yeye tu. na walipomuondoa akaenda kupata asilimia 48 za hapana,"

Akizungumzia kauli ya Mkuu wa Majeshi nchini, Jenerali Venance Mabeyo, Naibu huyo Waziri wa TAMISEMI amesema,"unaweza ukaona hivi Mkuu wa Majeshi ambaye anaangalia ulinzi wa nchi hii, hautaki atoe kauli za ulinzi wa nchi hii kweli?, kama kuna chokochoko ndani za uchochezi anaachaje?".

Hivi karibuni akizungumza kwenye uzinduzi wa Mji wa Serikali Wilaya ya Chamwino jijini Dodoma, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Venance Mabeyo alisema kwa sasa jeshi hilo linafuatilia baadhi ya kauli zenye utata zinazotokea ndani ya nchi ili kubaini kama zina viashiria vya uchochezi.