Ijumaa , 31st Jul , 2020

Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga ametoa siku 14 kwa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya nafaka na mazao mchanganyiko Dkt Anslem Moshi, kukamilisha malipo ya wakulima wote waliouza korosho msimu wa mwaka 2018/2019.

Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga.

Waziri Hasunga ametoa agizo hilo wakati alipotembelea na kukagua shughuli za utendaji kazi zinazofanywa na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko Jijini Arusha.

Amesema kuwa Bodi hiyo ilipewa dhamana ya kununua korosho mwaka 2018 kwa niaba ya Serikali na tayari imeshatoa fedha zote kwa ajili ya wakulima lakini bado CPB haijakamilisha malipo hivyo ni lazima malipo yakamilike ndani ya siku hizo.

“Ndani ya siku 14 sitaki kusikia malalamiko ya wakulima lazima wakulima wote wawe wamelipwa fedha zao haraka iwezekanavyo”, amesema Waziri Hasunga.

Akiwa kiwandani hapo Waziri Hasunga amebaini uchakavu wa mitambo iliyopo pamoja na uchache wa watumishi wanaofanya kazi katika kiwanda hicho, hivyo ameagiza kufanyika ukarabati wa majengo hayo kuanzia mwezi Agosti badala ya Oktoba kwa taasisi hiyo ilivyopanga.