Alhamisi , 2nd Apr , 2020

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema kuwa kutokana na uwepo wa maswali mengi ya wananchi kuhusu ugonjwa unaosababishwa na Virusi vya Corona, Wizara ipo tayari kuyajibu ambapo maswali yatakuwa yanajibiwa na Mkurugenzi wa Maabara ya Taifa ya Afya ya Jamii, Dkt. Nyambura Muremi.

Waziri wa Afya, maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu.

Taarifa hiyo imetolewa leo Aprili 2,2020, ambapo Waziri Ummy ameyataja baadhi ya maswali ambayo yamekuwa yakiulizwa, likiwemo lile la nani anakidhi vigezo vya kupimwa COVID-19, ambapo swali hilo limejibiwa na Dkt Muremi.

"Anayepaswa kupimwa ugonjwa wa COVID-19 ni yule aliyetimiza vigezo kama vile mtu kuwa na dalili za ugonjwa huo, kama mtu amepata kirusi, ataanza kuonyesha dalili kama vile kupata homa, hapa ndio tutanza kuchukua kipimo na huu ndio uthibitisho wa kisayansi,” amesema Dkt Muremi.

Akizungumzia taratibu za kupima ugonjwa huo kwa ngazi ya Mkoa Dkt Muremi amesema, "Baada ya kupima huko mikoani wanaleta sampuli Maabara ya Taifa ya Afya ya Jamii  ambayo ina vigezo vitatu vinavyotambulika Kimataifa ambavyo ni usalama wa kibailojia ngazi ya tatu (BSL-3).

Waziri Ummy amesema maswali, maoni na ushauri huo, unatoka kwa wananchi kupitia vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na kituo cha Wizara cha kupokea simu kuhusu ugonjwa wa homa inayosababishwa na Virusi vya Corona.