Jumanne , 9th Jun , 2020

Mbunge wa Iringa Mjini Mchungaji Peter Msigwa amesema kuwa, kabla ya watu wasiojulikana kumvamia na kumshambulia Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe, walimuambia kwamba yeye amekuwa akiisumbua sana Serikali na wala hawana mpango wa kumuua bali wanataka kumvunja tu.

Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe

Msigwa ameyabainisha hayo leo Juni 9, 2020, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma.

"Kuanzia saa 1 hadi saa 3 usiku tulikuwa wote, baadaye alipita maeneo ya karibu na kwangu akapaki gari yake, na walinzi wake waliondolewa kipindi kile cha sakata la Corona, kwa maelezo yake sasa wakati anapanda ngazi kwenda nyumbani kwake, wakashuka watu watatu wakiwa wamevaa makoti meusi wakamuambia wewe unaisumbua sana Serikali, tunataka tukuoneshe kama Serikali ipo, sisi hatuna mpango wa kukuua ila tunataka tukuvunje, ili ushindwe kufanya kampeni" amesema Mchungaji Msigwa.

Aidha Msigwa ameongeza kuwa "Ni aibu kubwa sana Wabunge kuushambuliwa tena kwa mara ya pili tukiwa bungeni tukifanya kazi ya wananchi, chama kinajipanga ili kutoka kwa wananchi kuongea na kujua nini msimamo wetu".