Jumanne , 15th Oct , 2019

Mbunge wa Kigoma Mjini na Kiongozi wa Chama cha ACT - Wazalendo, Zitto Kabwe amemuomba Waziri wa TAMISEMI, Selemani Jafo kuongeza siku zingine ili kutoa nafasi zaidi kwa wananchi kujitokeza katika zoezi la kujiandikisha kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Zitto Kabwe

Zitto ametoa kauli hiyo katika Kitongoji cha Kabinga, Mji Mdogo wa Mwandiga mkoani Kigoma, wakati akijiandikisha kwa ajili ya kupiga kura katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na kuwaomba viongozi kuacha kutoa vitisho na badala yake waongeze vishawishi kwa wananchi, kwani suala la kujiandikisha ni la utashi wa mtu binafsi.

''Namuomba Waziri wa TAMISEMI aangalie upya uamuzi wake wa kuongeza siku tatu bado ni chache, angalau uandikishaji ungekuwa wiki mbili, kwahiyo watafanya tathmini watatazama ili kuona kama wataweza kuongeza muda'', amesema Zitto.

Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Jafo, Oktoba 13, 2019 aliongeza siku tatu zingine kwa ajili ya wananchi kuendelea kujitokeza kujiandikisha katika daftari la kupigia kura viongozi wa Serikali za Mitaa, zoezi ambalo litafikia ukomo Oktoba 17 mwaka huu.