Jumanne , 25th Feb , 2020

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amesema kuwa hana mashaka na kuwa Rais Magufuli ataendelea kushikilia nafasi hiyo, kwani hana mpinzani kutokana na utendaji wake wa kazi.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda

Makonda ametoa kauli hiyo leo Februari 25, 2020, wakati akifungua mkutano wa Kamati ya ushauri ya Mkoa (RCC), uliowakutanisha Wabunge, Madiwani, Mameya pamoja na Wakuu wa Wilaya kwa lengo la kujadili na kutokomeza kero mbalimbali ndani ya Mkoa huo.

"Rais atakayeendelea kuongoza Taifa hili anajulikana, kuna siku nikamsikia mtu anajitangaza kule atachukua fomu ya kugombea Urais, nikasema wakimpitisha huyu kwenye chama chao mimi nitamuomba Dkt Magufuli nihangaike naye, huwezi ukamchukua Dkt Magufuli ukamshindanisha na kibaraka anayesimama kwenye jukwaa eti naye anagombea Urais wa nchi" amesema Makonda.

Hivi karibuni Mbunge wa Kigoma Mjini na Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe, alisema kuwa anayo nia ya dhati ya kugombea Urais na kuiongoza nchi, endapo wenzake wataridhia yeye kupeperusha bendera hiyo.