Jumatano , 16th Mei , 2018

Mwenyekiti wa Baraza la Vijana CHADEMA, Patrick Ole Sosopi amesema kwamba hawataki Mwanasheria wa chama chao, Tundu Lissu  akirudi Tanzania  awe mtu wa kuhudhuria kliniki kwa ajili ya matibabu bali wanatarajia aingie kwenye 'struggle' moja kwa moja.

Ole Sosopi ameyasema hayo leo wakati akijibu swali kwenye Kipindi cha KIKAANGONI kinachorushwa kila siku ya Jumatano kupitia ukurasa wa Facebook EATV,  na kuongeza kwamba wanatarajia kiongozi wao atarudi nchini mara tu atakapomaliza matibabu yake anayoendelea nayo huko nchini Ubelgiji.

"Tundu Lissu tunataka akirudi asirudi ku-atend clinic, aje aingie kwenye mapambano moja kwa moja. Lissu ni kama kaka kwangu, alipopigwa risasi nilifadhaika sana, mpaka kesho nawaza hawa watu walikuwa na dhamira gani" Ole Sosopi.

Aidha Mwenyekiti huyo ameongeza kuwa "Lissu ni 'asset' kwa Tanzania na Mungu amemponya kutuonyesha, na ndio maana yupo mpaka leo".  

Lissu ambaye ni Mbunge wa Singida Mashariki na Mwanasheria wa Chadema alipigwa risasi na watu wasiojulikana Septemba 7, 2017 alipokuwa kwenye maeneo ya nyumbani kwake Area D Jijini Dodoma wakati alipokuwa akirejea kutoka katika majukumu yake.