Jumatatu , 18th Jun , 2018

Msanii wa Bongo Fleva Rashidi Abdala maarufu kama Chid Benz anashikiliwa na Jeshi la Polisi Jijini Dodoma kwa tuhuma za kukutwa na dawa za kulevya aina ya Bhangi zinazodaiwa kufikia gramu tano (5)

Akizungumza na eatv.tv Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani Dodoma, Gilless Muroto amethibitisha kukamatwa kwa Chid Benzi na kusema kwa sasa yupo kituo cha kati ikiwa ni mara ya pili kukamatwa kwa msanii huyo ndani ya mkoa huo.

Aidha, Kamanda Muroto amesema wasanii watumie vyeo vyao kwa kufanya shughuli nzuri zinazowaingizia kipato na ziwe zinazokubalika na jamii na kisheria pia na sio kufanya biashara ambazo sio halali na zipo kinyume na sheria za nchi.

"Kwa mtu yoyote anaefanya biashara haramu kwa kuona yeye ni mtu fulani ajue sheria haichagui aina ya mtu au cheo ila sheria inafanya haki kwa kila mtu kama unakuwa na hatia basi sheria itakuadhibu", amesema Muroto.

Kwa upande mwingine, Kamanda Muroto amewataka wasanii kuwa makini, wasifanyishwe biashara na watu au wao kufanya biashara ambazo ni haramu pia wawe wa kwanza kuelimisha jamii na kupiga vita ya dawa za kulevya  na kupinga biashara zozote ambazo zipo kinyume na sheria.