Jumamosi , 19th Mei , 2018

Msanii wa Bongo Fleva mwenye 'hit song' ya 'Mvumo wa Radi' Alikiba amesema sababu kubwa ya yeye kukataa kumsaini mkongwe Abby Skillz katika 'label' yake ya 'King's Music' ni kutokana na mtu huyo hapo awali ndiye aliyemsaidia kuingia kwenye muziki hivyo isingekuwa heshima kufanya hivyo.

Alikiba ametoa ufafanuzi huo wakati alipokuwa anazungumza kwenye kipindi cha Planet Bongo ndani ya Heshima ya BongoFleva inayorushwa mubashara kupitia EATV baada ya msanii huyo kuiambia EATV kuwa yupo chini ya King's Music lakini kwa bahati mbaya muda ulipokwenda kidogo zikajitokeza taarifa kuwa hayupo tena ndani ya label hiyo jambo ambalo liliwachanganya watu na kutaka kujua ukweli wa jambo hilo ukoje.

"kiukweli niliweza kumsaini Abby Skillz kwenye label yangu ya King's Music lakini niliona simtendei haki kwasababu aliniingiza katika 'game' ya muziki na nikaweza kuona mwanga wa muziki wa bongo fleva kwa hivyo nikaona ni bora Abby ajitegeme yeye kama yeye", amesema Alikiba.

Pamoja na hayo, Alikiba ameendelea kwa kusema "kwasababu ukiwepo katika label ya King's Music lazima kuna asilimia pia zinakuwa zinatoka nini. Mimi sikutaka kumfanyia hivyo Abby, nilichokuwa nataka afanye muziki wake, ajisaidie yeye mwenyewe lakini tutakuwa naye pamoja katika kumsaidia kazi zake".

Alikiba amesema aliamua kuchukua maamuzi hayo kwa kuwa hakuona sawa kummiliki mtu ambaye aliweza kumsaidia kuingia katika muziki ambapo mpaka sasa anajulikana na kila mtu.