Jumanne , 5th Mar , 2019

Msanii wa Bongofleva Christian Bella ameongea kwa mara ya kwanza kuhusu picha zilizosambaa mitandaoni zikimuonyesha akiwa kwenye shughuli ya kufunga ndoa na kusema anaacha watu watafsiri walichokiona kwenye picha na si vinginevyo.

Christian Bella katika moja ya picha zilizozua mijadala mtandaoni.

Akiongea kwenye eNewz, Christian Bella amesema kitu walichokiona watu kama wameona ni ndoa basi ni ndoa na kama wameona ni video ya nyimbo basi waendelee kuona hivyo lakini  Bella hakutaka kuweka wazi kwamba ni kweli ameoa au laa pamoja na kushindwa pia kukanusha taarifa hizo.

"Mwaka 2019 ni mwaka wa kuoa na kuolewa wasanii wengi wamefunga ndoa, hivyo sio ajabu na sio vibaya mtu kuamua kufunga ndoa kwa maana mtu huwezi tu kakaa kama bachela muda wote andapo umri wako unakuwa umeruhusu kuwa mume wa mtu ikifika wakati muafaka nitawaambia ila kwa sasa wao waone picha na waichukulie poa kama ilivyo", Aliongea Christian Bella.

Pia Christian Bella amemalizia kwa kusema kwa sasa hana mpango wa kuachia nyimbo mpya kwani bado anajipanga kutokana na kile anachokisema kwamba anafanya 'show' nyingi kuliko wasanii wote hapa bongo hivyo hana haraka na kutoa nyimbo.