Alhamisi , 21st Feb , 2019

Msanii wa muziki wa hip hop bongo, Fareed Kubanda au Fid Q, amewaweka wazi watu waliokimbia na pesa za michango ya rambi rambi kwenye msiba wa msanii mwenzao, Godzilla.

Akizungumza ndani ya Planet Bongo ya East Africa Radio, Fid Q amesema kwamba wachangishaji walikuwa wengi, lakini baadhi ya michango ilifika ikiwemo iliyokusanywa na Niki Mbishi, Soggy Dogy na Wakazi, lakini wale waliochangisha kwenye vidaftari kuna baadhi hawakufikisha kabisa pesa hizo za rambi rambi.

“Kwa taarifa nilizotoka nazo kule watu ambao wamefikisha ni washakaji zetu tu wale ambao walichangisha ka njia ya simu, kule twitter, ambao wamewasilisha ni kina wakazi na Niki mbishi, kulikuwa na wachangishaji wengi, kulikuwa wenye vidaftari, sasa wale wenye vidaftari kuna ambao walifikisha na kuna wengine hawajafikisha kabisaaa”, amesema Fid Q.

Kutokana na hayo Fid Q amesema watu hao bado wana nafasi ya kuzirudisha na kuwasilisha kwa familia ya Godzilla, lakini wasipofanya hivyo Mungu ndiye atawahukumu.

Wito wangu kwa wote ni sawa tu kupita na rambi rambi, wajue ile ni rambi rambi watu wametoa kusaidia pale palipopungua, kwa hiyo bado muda wanao, watumie fursa hii kurudisha kisichokuwa chao, na kama hawatarudisha basi tumuchie aliyeumba wahukumu yeye”, amesema Fid Q.

Hivi karibuni tasnia ya Bongo Fleva ilipatwa na msiba wa msanii mwenzao Godzilla, ambaye alifariki Februari 13, baada ya kuugua ghafla.