Jumatatu , 16th Apr , 2018

Msanii wa muziki wa kizazi kipya , Dully Sykes, ametoa ya moyoni baada ya kutoalikwa harusi ya msanii mwenzake Alikiba, ambaye kwa asilimia kubwa amehusika kwenye sanaa yake ya muziki mpaka kufikia alipo sasa.

Akizungumza na Big Chawa wa Planet Bongo ya East Africa Radio, Dully Sykes amesema hajapewa taarifa yoyote kutoka kwa Ali Kiba licha ya kuwa mtu wake wa karibu, zaidi ya kuona mitandaoni na kuthibitishiwa na watu wa Mombasa.

“Mimi hajaniambia chochote na wala sijui, nimeona tu mitandaoni na nimepigiwa simu na dada yangu kutoka Mombasa, amenitaarifu kwamba Ali anaenda kuoa kule, lakini Ali hajaniambia chochote, mimi ni mtu ambaye nilikuwa namsapoti na ndiye nilianza kumkubali, kipindi hiko hakuna mtu yeyote anayemjua Ali Kiba, hata nyumba ya jirani hawamjui kama msanii, na niliposikia sauti yake tu nikamuomba collabo”, amefunguka Dully Sykes.

Hata hivyo Dully Sykes amesema anamtakia Alikiba maisha mema kwenye ndoa yake, kwani ni jambo la heri na kumsihi asichukulie mzaha suala la ndoa.

“Namtakia ndoa njema, nampenda sana na anajua, namtakia maisha mema, na namsihi ndoa sio kitu kidogo, anapoamua kuchukua mtoto wa watu, hasa ambaye amemchukua nchi nyingine, inabidi amuheshimu sana, amuonyeshe upendo hata yule mtoto akiitwa na wazazi wake mbona huji kutuangalia akose cha kuwaambia kwa upendo atakaompa”, amesema Dully

Hivi karibuni kumekuwa na taarifa kuwa Alikiba anatarajia kuoa hivi karibuni, ndoa ambayo imetangazwa kufanyika kwa siri nchini Kenya mjini Mombasa, na mpaka sasa mwanamke anayetarajia kuolewa na Alikiba hajajulikana ni nani kwa picha.