Jumatatu , 19th Mar , 2018

Mtayarishaji wa muziki wa BongoFleva nchini, Nisher Bybee amesema hakuna kikwazo chochote alichokipata wakati anaandaa video ya msanii Dogo Janja, 'Wayuwayu' na kudai pengine mke wake Irene Uwoya ndio aliyesababisha kuwepo hivyo.

Nisher ametoa kauli hiyo wakati alipokuwa anazungumza kwenye kipindi cha 'FRIDAY NIGHT LIVE' (FNL) inayorushwa na tinga namba moja kwa vijana EATV baada ya kuulizwa na swali na mtangazaji wa kipindi hicho kuwa ni tabu zipi alizipitia pindi alipokuwa anamuongoza Dogo Janja katika video ya wimbo huo ambayo amevaa uhusika wa mwanamke ambayo imekuwa gumzo mjini kwa jinsi rapa huyo alivyoabisha wana wa Arusha kwa mujibu wa maoni ya watu.

"Nilipigiwa simu na Madee kuwa anataka ku-shoot video mpya ya Dogo Janja lakini anataka aonekane yeye kama yeye, mimi nikaichukulia kama 'challenge' kwa kuwa sio kitu rahisi sana kukifanya lakini nikachukulia kama kazi na imekuja kutokea kitu kikubwa hata mwenyewe sikutegemea",amesema Nisher.

Pamoja na hayo, Nisher ameendelea kwa kusema "sasa sijui ni mke wake 'Irene Uwoya' ndio anamsababisha kuwa hivyo au vipi lakini Dogo Janja alikuwa anafanya vizuri kila 'shoot' tuliyokuwa tunafanya, hajanipa tatizo lolote la kurudia rudia ila kiukweli ni muigizaji mzuri wa pande zote"

Kwa upande mwingine, Nisher amesema licha ya kupewa lawama nyingi na baadhi ya watu ila anajivunia kuwepo kufanya kazi na Janjaro kwa kuwa amefanya ubunifu wa hali ya juu katika sanaa yake ya muziki kwa kuwa sio jambo rahisi kwa watu wengine kufanya hivyo.