Jumanne , 25th Sep , 2018

Binadamu huitaji mazingira mapya katika kupumzisha akili yake baada ya kufanya shughuli mbalimbali kwa muda mrefu, wengi hutembelea miji mbalimbali aidha kwa shughuli za kiutalii ama katika mihangaiko ya kazi.

Kampuni ya Mastercard imetoa listi ya miji mbalimbali ambayo imeongoza kwa kutembelewa zaidi mpaka sasa ndani ya mwaka 2018, ambapo mji wa Bangkok kutoka nchini Thailand umeendelea kubakia katika nafasi za juu kutoka mwaka uliopita, ikiwa na ukuwaji wa uchumi kwa asilimia 9.7.

Hii hapa ni listi ya miji 10 ambayo inaongoza kwa kutembelewa zaidi duniani mpaka sasa ndani ya mwaka 2018.

Bangkok, Thailand

Mji huo ambao umekuwa  maarufu kwa miaka mingi kutokana na vyakula vyenye viungo mbalimbali na mahekalu ya jamii ya Buddhi, umetembelewa na watu zaidi ya 21.9 millioni kutoka nje ya nchi ndani ya mwaka huu. Lakini hivi sasa inatajwa kuwa watu wanatembelea zaidi kwaajili ya manunuzi ya vitu mbalimbali yakiwemo ya vitu vya thamani. Duka maarufu la bidhaa nchini humo linalojulikana kama 'Siam Paragon shopping mall' , ni eneo ambalo liliwahi kuwa la pili kwa umaarufu katika mtandao wa Istagram kwa takwimu ya mwaka 2013.

London, Uingereza

Mji huo umetembelewa na watu zaidi ya 20.4 millioni mpaka sasa katika mwaka huu huku baadhi ya vitu vinavyowavutia watu wengi katika mji huo ni pamoja na matukio ya kimichezo ikiwemo ligi ya kuu ya nchi hiyo (EPL) ambayo ni ligi maarufu duniani, daraja lijuliakanalo kama 'Tower Bridge' ambalo lina historia tangu karne ya 19, 'London Eye' na kwaajili ya manunuzi mbalimbali.

Paris, Ufaransa

Mji huo umeshatembelewa na watu 17.9 millioni mpaka sasa katika mwaka 2018 ambapo kivutio kikubwa ni mnara wa Eiffel ambao unashikilia historia ya kuwa moja kati ya minara mrefu zaidi duniani. Vivutio vingine vinavyowavutia watu wanaotembele mji huo ni katika matukio ya kimichezo, kama mashindano ya Tenisi ya French Open na michezo ya soka ya ligi ya Ufaransa, Ligue 1.

Dubai, UAE

Mji huo umetembelewa na watu takribani 16.6 millioni mpaka sasa ndani ya mwaka 2018 ambapo wengi kati hao wametembelea kwaajili ya shughuli za utalii ikiwemo kutazama madhari ya mji huo ambao umejengwa kwa ustadi wa hali ya juu pamoja na kufanya manunuzi mbalimbali ya vitu vya thamani hasa vyevye tamaduni za kiarabu ambapo wastani wa matumizi ya wageni hao kwa mwaka huu ni dola 537 kwa siku ambayo ni sawa na 1.2 millioni za kitanzania.

Singapore

Visiwa hivyo vimevutia watu takribani 14.4 millioni mpaka sasa. Watu wengi wanavutiwa na utalii katika visiwa hivyo ambapo maeneo yanayovutia watu wengi ni kama Singapore zoo, makumbusho ya visiwa hivyo yakiwemo mahekalu ya kibuddha, kilele cha mlima Faber ambacho kinaonesha kwa ufasaha maemeo yote ya mji, eneo maarufu la kuogelea la 'Jurong East' na maeneo mengine mengi.

Miji mingine iliyotembelewa na watu wengi mpaka sasa duniani ni pamoja na New York(Marekani) ambao umetembelewa na watu 13.6 millioni, Kuala Lumpur(Malaysia) ukiwa na idadi ya watu 13.5 millioni waliotembelea, Istanbul(Uturuki) ukitembelewa na watu 12.8 millioni, Tokyo(Japan) wenye watu 12.2 millioni waliotembelea pamoja na Antalya(Uturuki) uliotembelewa na watu 11.2 millioni mpaka sasa.