Jumatatu , 8th Apr , 2019

Kijana Brighton Moyo, raia wa Zimbabwe aliyekuwa akiishi Afrika Kusini ambaye alijipatia umaarufu baada ya kuonekana katika tukio la kufufuliwa na Mchungaji Alph Lukau, amefariki Dunia na amezikwa Jumamosi iliyopita.

Mchungaji Alph Lukau akiwa na marehemu Brighton.

Kwa mujibu wa majirani zake kutoka nchini humo wanadai kuwa alizikwa siku tatu baada ya kufariki, na inaelezwa kuwa alikuwa akiishi na VVU, na baadaye figo na mapafu yake vilishindwa kufanya kazi hadi hapo vilipopelekea kifo chake.

Mmoja kati ya ndugu zake amesema kuwa walipewa na taarifa za ugonjwa wake na msichana aliyekuwa akiishi naye ambaye aliwaeleza kuwa, tumbo lake lilianza kuvimba na kujaa maji na baada ya siku tatu akawa amefariki.

Kijana huyo alijizolea umaarufu baada ya kusambaa kwa habari za Mchungaji wa Afrika Kusini Alph Lukau kumfufua mtu katika ibada yake ya Jumapili ya Februari 24, 2019, ambapo baadaye iligundulika kuwa hakuwa amefariki.