Alhamisi , 11th Oct , 2018

Jopo la madaktari nchini India wamefanikiwa kuondoa mnyoo mwenye urefu wa Sentimita 15 kutoka kwenye jicho la mwanaume mmoja nchini humo kufuatia oparesheni iliyofanyika.

Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 60 ambaye jina lake halijajulikana, alikuwa akisumbuliwa na tatizo la macho kuuma  kwa muda mrefu ndipo alipoamua kwenda kuwaona madaktari hao.

Oparesheni hiyo imefanyika katika jimbo la Karnataka linalopatikana kusini magharibi mwa nchi hiyo, ambapo katika uchunguzi zaidi wa madaktari uligundua kuwa mgonjwa huyo aliathiriwa na minyoo hadi katika damu yake.

Mmoja wa madaktari waliohusika katika oparesheni hiyo, Dr.Srikanth Shetty amesema,

'" Changamoto ilikuwa ni kumtoa mnyoo huyo mzima, kuepuka kufia katika jicho la mgonjwa huyo, jambo ambalo lingeleta matatizo makubwa zaidi ".

" Na ilikuwa ni ngumu kumbana mnyoo huyo kwasababu alikuwa akitembea tembea katika jicho la mgomjwa. Pia tumegundua kuwa alikuwa na minyoo hadi kwenye damu na tumempatia matibabu yake", ameongeza daktari huyo.

Kwa makadirio, takribani watu millioni 120 katika nchi za Afrika ya kati, kusini na katikati ya bara la Amerika  pamoja na bara la Asia wanaugua magonjwa ya minyoo lakini ni mara chache hutokea minyoo hiyo kuvamia katika macho.

Katika tukio lingine nchini Malaysia, raia mmoja alijikuta katika dalili hizo za macho baada ya kuogelea katika mto wiki kadhaa zilizopita.