Alhamisi , 9th Aug , 2018

Klabu ya African Lyon imetambulisha rasmi kocha mpya na mchezaji wa kigeni katika mazoezi ya kwanza ya timu hiyo yaliyofanyika leo katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Kocha (kulia) pamoja na mchezaji (Kushoto) kwenye utambulisho katika uwanja wa Uhuru

Kocha aliyetambulishwa ni, Soccoia Lionel raia wa Ufaransa pamoja na mchezaji alieambatana naye, Victor Da Costa ambapo wote kwa pamoja wamesaini mkataba wa miaka miwili kila mmoja kuitumikia klabu hiyo.

Akizungumzia utambulisho huo, meneja wa klabu hiyo, Adam Kipatacho amesema kuwa African Lyon ni moja ya klabu zilizofanya usajili mzuri kwa klabu za ligi kuu msimu huu japokuwa haizungumziwi miongoni mwa wadau wa soka.

Naye kocha mpya wa timu hiyo amesema kuwa amejipanga vizuri kuhakikisha African Lyon inafanya vizuri katika ligi kuu msimu huu.

Soccoia amefundisha vilabu kadhaa barani Afrika vikiwemo, CIFAS ya Benin na Cotton Sports ya Cameroon.

African Lyon imepanda daraja msimu huu na inatarajia kucheza mechi yake ya ufunguzi wa ligi, Agosti 23, dhidi ya Stand United katika uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga.