Jumatatu , 9th Jan , 2017

Wakati michuano ya Kombe la Mapinduzi ikiingia katika hatua ya nusu fainali huku bingwa mtetezi timu ya URA ya Uganda wakifungashwa virago, tayari timu ya Azam imetabiriwa kuchukua ubingwa wa michuano hiyo kwa mwaka huu.

Kikosi cha Azam FC

Mtu wa kwanza kufanya hivyo ni nahodha wa URA, Jimmy Kulaba, ambaye amesema kuwa baada ya wao kutupwa nje, timu pekee yenye uwezo wa kunyakua kombe hilo mwaka huu ni Azam FC ya Dar es Salaam.

Jimmy alitoa utabiri wake jana usiku mara baada ya kumalizika kwa mchezo wao dhidi ya Taifa Jang'ombe ambao ulimalizika kwa URA kufungwa bao 1-0, na kuvuliwa rasmi ubingwa wa micuano hiyo.

Jimmy amesema kwa jinsi alivyokiona kikosi cha Azam kilichoshinda mabao 4-0 dhidi ya Yanga, anaona hakitakuwa na mpinzani katika timu zote nne zilizotinga nusu fainali.

Jimmy Kulaba

"Azam wa kikosi kizuri, wachezaji wake ni wazoefu, wanajitambua na wako serious na kazi, natamani kuona Azam wanakuwa mabingwa wa Mapinduzi"

Azam wanakutana na Taifa Jang'ombe katika moto wa nusu fainali ya kwanza utakaopigwa kesho Jumanne saa 10 jioni, wakati mchezo wa pili wa nusu fainali utazikutanisha Simba na Yanga saa 2 usiku.

Je, utabiri huu utatimia, tusubiri