Jumapili , 24th Mar , 2019

Kocha wa timu ya taifa ya Uganda, Sébastien Desabre amezungumzia maandalizi yao kuelekea mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi dhidi ya Taifa Stars, saa 12 jioni katika uwanja wa taifa.

Kocha wa Uganda, Sebastian Desabre (kushoto) na kikosi cha Taifa Stars.

Akizungumza katika mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo, Desabre amesema kuwa anajua kuwa wao wameshafuzu michuano ya AFCON na wanachotakiwa ni kuendeleza hatua hiyo.

"Maendeleo ya timu yetu katika hatua zinazofuata ni mazuri, tumekuwa ni miongoni mwa timu za kwanza kufuzu na kesho tutakuwa tunaendeleza maandalizi yetu ya hatua inayofuata ya AFCON", amesema kocha Desabre.

"Tanzania ina timu nzuri na kocha mzuri pia, tumeiona hata katika mchezo tuliocheza nao nyumbani. Najua kuwa wako katika 'pressure' kubwa ya kufuzu na kwa upande wetu tuna pressure ndogo lakini huu ni mchezo wa kimataifa, tutaonesha ushindani hata kama mchezo hautakuwa na faida sana kwetu", ameongeza.

Moja ya mechi kati ya Uganda Cranes na Taifa Stars

Kwa upande wake nahodha wa timu ya taifa ya Uganda, Denis Onyango amesema kuwa mchezo dhidi ya Taifa Stars kwao una umuhimu mkubwa huku akiita ni 'Derby' ya Afrika Mashariki.

"Tunajiandaa na michuano ya AFCON, mchezo wa kesho (leo) utakuwa ni wa kuvutia sana, itakuwa ni Derby ya Afrika Mashariki. Kama ilivyo kwao wanahitaji ushindi na sisi pia tunahitaji kushinda kwahiyo utakuwa ni mchezo mzuri kwetu kwaajili ya maandalizi kuelekea michuano hiyo", amesema Onyango.

Taifa Stars inahitaji ushindi ili iweze kufuzu wakati huohuo ikiiombea matokeo mazuri Cape Verde kwenye mchezo wake dhidi ya Lesotho.

Bonyeza hapa chini kutazama zaidi.