Jumatatu , 18th Feb , 2019

Mshambuliaji wa klabu ya soka ya Simba, Meddie Kagere kwasasa ndiye shujaa wa timu na huenda asipendwe sana na mashabiki wa timu pinzani kutokana  na namna anavyoziadhibu timu zao msimu huu.

Meddie Kagere akiwa na wachezaji wa Al Ahly katika mchezo uliopigwa Dar es salaam.

Kagere msimu huu ndiye kinara wa mabao msimbazi mpaka sasa ambapo anaongoza kwenye ligi kuu Tanzania bara na pia kwenye Ligi ya mabingwa Afrika.

Katika mechi tatu zilizopita, Simba imefunga mabao matano. Mabao 3-0 dhidi ya Mwadui FC, 1-0 dhidi ya Al Ahly na 1-0 dhidi ya Yanga.

Kati ya hayo matano Meddie Kagere amefunga matatu kwa wastani wa goli moja katika kila mchezo.

Kwenye ligi kuu Kagere ana mabao 9 na anaongoza kwenye klabu yake akifuatiwa na Emmanuel Okwi mwenye mabao 7. Kwa ujumla Kagere sasa yupo nyuma ya Eliud Ambokile mwenye mabao 10 na Heritier Makambo mwenye mabao 11.

Kwa upande wa Ligi ya Mabingwa Afrika Kagere ana mabao manne na anashika nafasi ya pili nyuma ya Jean-Marc Makusu wa AS Vita Club mwenye mabao matano.

Kagere ambaye alisajiliwa msimu uliopita kutoka klabu ya Gor Mahia ya Kenya, yupo jijini Arusha na kikosi cha Simba ambapo kesho watashuka dimbani kucheza na African Lyon kwenye mchezo wa ligi kuu.