Jumanne , 12th Feb , 2019

Kuelekea mchezo wa Simba leo dhidi ya Al Ahly ambao ni wa nne kwa kila timu katika kundi D ligi ya mabingwa Afrika, viongozi mbalimbali wameitakia heri Simba katika mchezo huo.

Kushoto ni Tulia Ackson na kulia ni Mwigulu Nchemba

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh Tulia Ackson ambaye pia alikuwa mgeni rasmi katika mchezo wa kwanza wa Simba katika kundi hilo dhidi ya JS Sauora ambapo Simba ilishinda 3-0, amesema timu hiyo ina kila sababu ya kushinda tena.

''Nguvu tunayo, uwezo tunao na nia tunayo. Leo tuna kila sababu ya ushindi. Kila la heri Simbasc Tanzania'' ameandika Tulia Ackson.

Kwa upande wake waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani na mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba, ameweka wazi kuwa anaungana na Simba kuhakikisha timu hiyo inaiwakilisha vizuri nchi na kushinda mchezo huo.

Kwa upande wa wachezaji wa Simba kiungo Clatous Chama amesema muungano na nguvu ya pamoja kutoka kwa wachezaji ndio huleta ushindi ndani ya Simba na anaamini hilo litatoekea leo.

Wakati huo mshambuliaji wa kikosi hicho Meddie Kagere amesema wamejiandaa vizuri kwa mchezo huo na wapo tayari kwa mapambano kuhakikisha wanashinda.

Mchezo huo unaanza saa 10:00 jioni kwenye uwanja wa taifa Dar es salaam.