Alhamisi , 9th Aug , 2018

Msimu mpya wa ligi kuu nchini Uingereza (EPL), unatarajia kuanza kesho Ijumaa kwa mchezo mmoja wa ufunguzi kati ya Manchester United na mabingwa wa msimu wa 2015/16, Leicester City.

Wachezaji wanaopewa nafasi ya kushinda tuzo ya mfungaji bora wa EPL msimu huu

Kuelekea ufunguzi wa msimu mpya wa EPL, tunaangazia wachezaji ambao wanapewa nafasi ya kuibuka wafungaji bora wa ligi hiyo msimu huu kutokana na rekodi zao za kufumania nyavu kwenye misimu kadhaa iliyopita.

Mohamed Salah, Alifunga jumla ya magoli 44 katika mashindano yote msimu uliopita ambapo 32 kati ya hayo ni ya EPL na kuibuka mshindi wa kiatu cha dhahabu, anaweza kurudia tena moto huo msimu huu kutokana na kiwango chake katika mechi za maandalizi ya msimu alizocheza mpaka sasa.

Harry Kane, Kijana huyo Muingereza alifunga magoli 30 ya EPL Msimu uliopita, mawili nyuma ya kinara, Mo Salah. Majeraha aliyoyapata katikati ya msimu uliopita yalimrudisha nyuma kasi yake ya kufunga, lakini sasa yuko vizuri, ameshinda tuzo ya mfungaji bora wa michuano ya kombe la dunia iliyomalizika nchini Urusi na huenda msimu ujao akafanya makubwa na kushinda tuzo hiyo kama alivyofanya mara ya mwisho msimu wa 2016/17.

Sergio Aguero, Amekuwa thabiti katika ufungaji kwa misimu minne sasa, akifunga magoli si chini ya 20 kila msimu, msimu uliopita alifunga magoli 21 licha ya kubadilishana nafasi ya kuanza kikosi cha kwanza na mchezaji chipukizi Gabriel Jesus. Aguero ataiongoza tena Man City msimu huu inayopewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa wa EPL kwa mara ya pili mfululizo.

Jamie Vardy, Amekuwa na misimu bora sana tangu alipopanda na Leicester City kwenye ligi kuu ya EPL msimu wa 2014/15, alifunga jumla ya magoli 20 msimu uliopita na endapo ataongeza ubora wa kasi yake na umakini wa kufunga kwenye msimu huu anaweza kuwa ni mshindani wa tuzo hiyo.

Romelo Lukaku, Alifunga magoli 16 pekee msimu uliopita huku kinara akiizidi mara mbili idadi yake, anayo nafasi kubwa ya kuibuka mshindi wa kiatu cha dhahabu msimu huu endapo atatumia vizuri nguvu na kasi alivyonavyo katika kutafuta magoli.

Pierre-Emerick Aubameyang, Alijiunga na Arsenal mwezi Januari mwaka huu na kufanikiwa kufunga magoli 10 katika mechi 13 za EPL alizocheza , akipata nafasi ya kucheza mechi nyingi msimu ujao anaweza kufungunga magoli mengi zaidi yatakayomsaidia kuibuka na ushindi wa tuzo hiyo.