Alhamisi , 22nd Jul , 2021

Mshambuliaji wa Klabu ya soka ya Yanga, Saido Ntibazonkiza ataukosa mchezo wa Fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam Sports Federation Cup wakati timu yake itakapomenyana na Simba siku ya Jumapili Julai 25,2021 kutokana na kuwa majeruhi.

Mshambuliaji wa Yanga, Saido Ntibazonkiza(Pichani) akiwa mazoezini kabla ya kupata makeraha.

Afisa Muhamasishaji na Msemaji wa Yanga, Antonio Nuggaz ameiambia East Africa Radio kuwa Ntibazonkiza aliumia misuli ya paja akiwa mazoezini hivyo ndiye mchezaji pekee watakayemkosa katika mchezo huo.

''Tutamkosa Saido Ntibazonkiza pekee kwakuwa aliumia jana mazoezini misuli ya paja, lakini wachezaji wengine wote wapo vizuri kiafya na tunatarajia kuwa na mchezo mzuri siku ya Jumapili''

Yanga imewasili mapema leo Mkoani Kigoma tayari kwa Fainali hiyo ambayo itachezwa kwenye uwanja wa Lake Tanganyika majira ya saa 9 Alasiri.