Jumatatu , 11th Mar , 2019

Kuelekea mchezo wa kesho wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kati ya Juventus ya Italia dhidi ya Atletico Madrid ya Hispania, mshambuliaji Cristiano Ronaldo, anafikiria timu yake itafanya yaliyofanywa na Man United dhidi ya PSG.

Cristiano Ronaldo

Akiongea leo na tovuti ya klabu, Ronaldo amesema wapo tayari kwa 'Come back' na anaamini watafanya hivyo kwa kutokea nyuma kwa mabao 2-0 waliyofungwa wiki kadhaa zilizopita walipoitembelea Atletico Madrid.

"Mimi pamoja na wenzangu kwenye timu tupo tayari kwa mchezo huu mzuri na utakuwa usiku maalumu kwetu ndani ya uwanja na kwa mashabiki pia jukwaani'', amesema.

Ronaldo amesisitiza kuwa mashabiki wanatakiwa wawaamini na kuwapa nguvu muda wote watakapokuwa uwanjani wafikirie zaidi kuwa tunafanya 'Come back'.

Wiki iliyopita timu za Ajax na Man United zilishangaza wapenzi wa soka duniani kwa kupindua matokeo baada ya Man United kushinda 3-1 nyumbani kwa PSG huku Ajax wakishinda 4-1 Santiago Bernabeu.