Alhamisi , 16th Aug , 2018

Timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 17 ya Tanzania, Serengeti Boys imeibuka na ushindi mnono wa mabao 5-0 dhidi ya timu ya vijana ya Sudan katika mfululizo wa michezo ya kufuzu fainali za AFCON za vijana U-17 kanda ya Afrika Mashariki zinazoendelea hapa nchini.

Serengeti Boys wakishangilia ushindi

Mchezo huo uliofanyika katika uwanja wa taifa na kuhudhuriwa na mashabiki wengi waliojitokeza kuja kuisapoti timu yao, ulianza kwa kandanda safi katika kipindi cha kwanza huku kila timu ikicheza kwa umakini mkubwa.

Serengeti Boys ndiyo walikuwa wakwanza kupata bao dakika ya 19 kupitia kwa Edson Mshirakandi aliyepiga kona ya moja kwa moja na kumshinda mlinda mlango wa Sudan, Omer Miso, bao lilidumu hadi mapumziko.

Kipindi cha pili Serengeti Boys waliamka zaidi na kucheza mpira wa kuvutia mbele ya mashabiki wao ambao waliwashangilia kwa hari zaidi, mabao mengine yalifungwa na Kelvin John dakika ya 45 na 60 pamoja na Agiri Ngoda dakika ya 72 na 79.

Kwa ushindi huo Serengeti Boys inafikisha alama 6 kwa kushinda michezo yake yote miwili, mchezo wa kwanza ilishinda mabao 2-1 dhidi ya Burundi, Timu zingine zenye alama sita ni Rwanda na Ethiopia zote zikiwa baada ya kushinda michezo yake miwili.