Alhamisi , 14th Nov , 2019

Klabu ya Simba imebainisha tarehe ambayo itazindua uwanja wake wa mazoezi uliopo Bunju Jijini Dar es Salaam.

Uwanja wa Simba uliopo Bunju

Hayo yamebainishwa na Katibu wa klabu hiyo, Anold Kashembe huku akieleza sababu zinazopelekea kutozinduliwa mapema kwa uwanja huo kama ambavyo ilitajwa awali.

Kashembe amesema kikubwa kinachokwamisha kukamilika kwa uwanja huo ni kutokana na mvua zisizoeleweka kuendelea kunyesha mara kwa mara, ambapo ameahidi kuwa mpaka kufikia Disemba 7, uwanja huo utakuwa umekamilika.

Kuna mvua ambayo imenyesha hapa kati ndiyo imetibua hasa katika ule uwanja wa nyasi bandia ambapo ule udongo umevurugika, lakini upande wa nyasi asilia mambo yanakwenda vizuri. Kutokana na hilo, tarehe 7 ya mwezi ujao, kabla ya mkutano mkuu haujafanyika tunatarajia kuuzindua rasmi uwanja wetu huu.", amesema Kashembe.

Simba lianza kujenga uwanja wao wa mazoezi ambapo awali ulitarajiwa kumalizika Februari mwaka huu, lakini changamoto zilizojitokeza zikakwamisha ujenzi huo ambao sasa imetangazwa utakuwa sawa Desemba, mwaka huu na Mkutano Mkuu wa klabu hiyo unatarajiwa kufanyika Desemba 8 mwaka huu.