Ijumaa , 23rd Mar , 2018

Mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Njombe Mji na Simba SC uliokuwa umeahirishwa hapo awali sasa umepangwa kufanyika mnamo Aprili 3, 2018 katika uwanja wa Sabasaba mkoani Njombe.

Hayo yamebainishwa na taarifa zilizotoka ndano ya bodi ya ligi na kusema kwamba tayari timu zote mbili zimekwishapatiwa taarifa kwaajili ya maandalizi ya mchezo huo.

Awali kwa mujibu wa ratiba ya ligi hiyo, mchezo huo ulikuwa umepangwa kuchezwa Machi 11 mwaka huu, lakini ukaahirishwa ili kuipa Simba nafasi ya kufanya maandalizi ya mchezo wake wa marudiano dhidi ya Al Masry katika michuano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika ambapo Simba walitolewa kushiriki mashindano hayo baada ya kulazimishwa kutoka sare ya bila ya kufungana katika mchezo huo.

Kwa upande mwingine, Bodi ya ligi bado haijapanga tarehe kwaajili ya michezo miwili inayoihusu timu ya Mtibwa Sugar ya Morogoro, dhidi ya Simba na Yanga ambayo pia iliahirishwa kutokana na timu hizo mbili za jijini Dar es Salaam kukabiliwa na majukumu ya Kimataifa.