Jumatano , 20th Feb , 2019

Mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania Bara klabu ya Simba, inajaribu kupambana kwa kila namna kuhakikisha inakwenda sambamba na ratiba ya viporo vyake ili ifanye vizuri.

Kikosi cha Simba

Baada ya mchezo wake dhidi ya African Lyon jana jijini Arusha, tayari timu hiyo imerejea jijini Dar es salaam na hakuna kupumzika ambapo jioni ya leo kikosi kinaanza mazoezi tayari kwa mchezo ujao dhidi ya Azam FC.

Taarifa ya Simba imefafanua kuwa, ''Kikosi chetu tayari kimerejea jijini Dar es Salaam, na leo jioni kitaanza mazoezi kujiandaa na mchezo ujao wa Ligi Kuu''.

Simba inakabiliwa na michezo mfululizo ya ligi kuu pamoja na Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo baada ya kumalizana na African Lyon sasa inaisubiri Azam FC 22/02/2019.

Baada ya mchezo huo kesho yake inasafiri kwenda Iringa na inakuwa na siku 2 za mazoezi ambapo itacheza 26/02/2019 dhidi ya Lipuli FC.

Kisha itaunganisha kwenda Shinyanga na itakuwa na siku 2 tu za mazoezi kabla ya 03/03/2019 kuivaa Stand United.

Baada ya mechi hiyo Simba itarudi Dar es salaam kwa ajili ya maandalizi ya safari ya kwenda Algeria 06/03/2019 ambapo itasafiri kwenda kucheza na JS Saoura Machi 9/2019.