Jumatano , 15th Aug , 2018

Uongozi wa Singida United umekana kuwa na mahusiano na klabu ya Yanga baada ya taarifa kusambaa kuwa klabu hiyo imewatoa baadhi ya wachezaji wake iliyowasajili msimu huu bure kwenda klabu ya Yanga.

Wachezaji wa Singida United na Yanga wakichuana katika moja ya mchezo wa ligi kuu.

Akizungumza katika tukio la kutambulisha udhamini mpya wa vifaa vya michezo vya msimu huu vya timu hiyo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Singida United, Festo Sanga amesema.

Kunapokuwa na urafiki wa mtu mmoja na klabu nyingine haimaanishi klabu yetu ina urafiki na timu hiyo, Singida United naweza nikasema haijawahi na haitokuja kutokea kujenga urafiki na Yanga kwasababu unapoleta urafiki kati ya timu hizi mbili ambao unafikia kiwango hadi cha kubadilishana wachezaji bure, inashusha ushindani kwenye ligi", amesema Sanga.

Sanga ameongeza kuwa katika kuthibitisha kuwa hawana urafiki na klabu ya Yanga, walifanya kila liliwezekana msimu uliopita ili kuwafunga Yanga na walifanikiwa katika hilo baada ya kuwatoka katika michuano ya shirikisho.

Katika hatua nyingine klabu hiyo imetambulisha jezi rasmi za nyumbani na ugenini watakazozitumia katika mashindano msimu huu, jezi ya nyumbani ikiwa na rangi ya bluu inayomaanisha kuenzi historia ya timu hiyo ambayo ilianzia katika ziwa Singidani.

Jezi ya ugenini ikiwa na rangi ya kijani na njano ambayo inalenga kuwakilisha zao maarufu la Alizeti linalolimwa kwa wingi mkoani Singida.