Jumamosi , 7th Mar , 2020

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa Na Michezo, Dkt. Hassan Abbasi amewaagiza maafisa wa Wizara yake kusimamia haraka mmarekebisho ya eneo mojawapo la benchi la wachezaji wa akiba kwenye Uwanja Mkuu wa Taifa Dar es Salaam baada ya kutoridhishwa na hali ya paa la benchi hilo.

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa Na Michezo, Dkt. Hassan Abbasi akiwa na maafisa wa Wizara yake.

Dkt. Abbasi aliyefika kukagua uwanja huo leo Jumamosi, uwanja utakaotumika kwa mechi ya watani wa jadi Simba na Yanga kesho Jumapili, ameeleza kuridhishwa na maandalizi ya uwanja huo lakini akashangaa eneo hilo la benchi kuwa na paa lililopasuka linaloweza kusababidhanwachezaji wa akiba kulowa mvua ikinyesha. 

Kutokana na hali hiyo, Dkt. Abbasi aliwahoji watendaji wa Wizara hiyo aliokuwa nao na kisha kumpigia simu papo kwa papo Mhasibu Mkuu wa Wizara hiyo na kumwagiza atoe fedha za marekebisho hayo leo leo.
 
"Nimefika hapa kujiridhisha na maandalizi ya uwanja huu utakaotumika kwa mechi ya Simba na Yanga hapo kesho ambao kimsingi ni wa Serikali lakini hili dogo la paa la benchi la wachezaji kupasukabna kuvuja nataka nikifika hapa kesho asubuhi  nikute limerekebishwa. Haya mambo madogo madogo tusiiache Serikali ikaaibika bila sababu. 

"Nimeshamwagiza Mhasibu Mkuu atoe fedha kufanya ukarabati mdogo wa eneo hili leo leo. Fuatilia," alisema Dkt. Abbasi akimwagiza Mkurugenzi wa Michezo, Yusuph Singo kufuatilia na kusimamia jukumu hilo. 

Awali Dkt. Abbas alifanya kikao cha ndani na watendaji wote wanaosimamia uwanja na mechi na kusisitiza kuwa Serikali inataka kuona watu wanafurahia mechi hiyo kwa amani lakini pia kusiwe na upotevu wa mapato  ya Serikali na pia kila mdau apate stahili yake.
 
Aidha, ametembelea maeneo mbalimbali ya uwanja huo na kusisitiza: "Nimeridhika. Maandalizi yako tayari na jukumu letu Serikali ni kuhakikisha kesho wote watakaofurahia baada ya matokeo na wale watakaohuzunika tunawalinda na kuwahakikishia usalama wao kabla, wakati na baada ya mechi.".