Alhamisi , 5th Mar , 2020

Uongozi wa klabu ya Yanga umesema kuwa unatarajia kutangaza mabadiliko makubwa ya klabu hiyo mara baada ya kumvaa mtani wao jadi Simba, Jumapili Machi 8, 2020.

Mashabiki wa Yanga

Mabadiliko hayo ni ya kimfumo wa uendeshaji wa timu, ikiwa ni kazi ya Kamati ya Mabadiliko pamoja na Mwenyekiti wa klabu hiyo, Dkt. Mshindo Msolla.

Hayo yameelezwa na Afisa Mhamasishaji na Msemaji wa klabu hiyo, Antonio Nugaz, akisema kuwa tayari mpango huo umekamilika kwa asilimia kubwa kwa ushirikiano wa pande zote mbili.

"Kuna jambo kubwa litafuata baada ya hiyo tarehe 8 Machi kumfunga mtani, tunatambulisha mchakato wa mabadiliko chini ya Kamati ya Mabadiliko pamoja na Mwenyekiti Dkt. Mshindo Msolla", amesema Nugaz.

Kuhusiana na mchezo huo mkubwa utakaopigwa katika uwanja wa taifa, Nugaz amesema kuwa wamejipanga vyema kushinda mchezo kutokana na uwezo wao lakini endapo hakutakuwa na makandokando ya uwanjani.