Ijumaa , 23rd Feb , 2018

Mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania Bara klabu ya Yanga inatarajiwa kuunganisha kesho asubuhi kwenda mjini Songea kucheza na Majimaji FC ikiwa ni siku moja tu tangu itue kutoka nchini Shelisheli.

Yanga SC ambayo imerejea nchini jana usiku ikitokea Shelisheli ambako ilicheza mchezo wake wa marudiano hatua ya awali ya ligi ya mabingwa Africa na kufuzu katika hatua ya kwanza, inakabiriwa na kibarua cha kombe la FA dhidi ya Majimaji FC.

Yanga itafanya maziezi leo jioni kwenye Uwanja wa Chuo cha Polisi Kurasini jijini Dar es Salaam kabla ya mapema kesho kusafiri kwa ndege kwenda Songea kwa ajili ya mchezo wa hatua ya 16 Bora michuano FA dhidi ya wenyeji wao Majimaji wikiendi hii.

Mbali na mchezo huo wa Yanga, hatua ya 16 Bora ya FA itaendelea pia kwa Singida United kuwakaribisha Polisi Tanzania kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida na KMC kumenyana na Azam FC Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.