Tuesday , 14th Jan , 2020

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda, amewataka Mashabiki wa Simba kuwa watulivu baada ya Mwekezaji, Mohammed Dewji kutangaza kujiuzulu kwenye nafasi ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba.

Makonda na Mo Dewji

Kauli hiyo ya Makonda imekuja baada ya Mohammed Dewji, kuandika kujiuzulu nafasi hiyo saa chache baada ya Simba kufungwa kwenye fainali ya Kombe la Mapinduzi dhidi ya Mtibwa kwa bao 1 - 0.

Makonda ameandika kuwa "natoa pole Kwa timu yangu ya Simba na Mashabiki wote na wanaoitakia mema Simba, sina uhakika na kinachoendelea kwenye akaunti ya MO kama ni Mo Dewji mwenyewe ameandika, nawaomba wanasimba tutulie tutapata ukweli muda si mrefu."

Katika tweet yake Mo Dewji ameandika kuwa "Ni aibu Simba kutoshinda, baada ya kulipa mishahara inayokaribia Bilioni 4 kwa mwaka, najiuzulu kama mwenyekiti wa bodi na kubakia muwekezaji, Simba Nguvu Moja, nitatia nguvu kwenye kuendeleza miundombinu na soka la vijana"