Saturday , 19th Sep , 2020

Kocha wa Klabu ya Simba, Sven Vandebroeck amesema kinachoendelea juu yake na mshambuliaji Meddie Kagere ni siri yake hawezi kuiweka hadharani.

Kocha Mkuu wa Simba Sven Vandebroeck ( wa kwanza kulia akiwa amekaa) akiwa na msaidizi wake Seleman Matola (Aliyesimama) mazoezini kwa pamoja.

Akizungumza katika Kipindi cha Kipenga kinachoruka kila siku za Jumatatu na Ijumaa saa 2-3 Usiku East Africa Radio,Pia Sven amedai kuwa kumuanzisha benchi mfungaji bora aliyefunga magoli zaidi ya ishirini kwa misimu miwili mfululizo ni jambo la kawaida.

''Masuala yangu na Meddie Kagere ni siri yangu siwezi kuyasema''

''20 kitu gani kwani Gonzalo Higuain mbona anakaa benchi japo alifunga magoli 30 na ni mshambuliaji bora''

Simba itashuka dimbani kwa Mkapa kesho kuikabili Biashara ya Mara, huku ikiwa imekusanya alama 4 katika mechi 2 za awali dhidi ya Ihefu na Mtibwa Sugar.

Kumekua na sintofahamu kuhusu matumizi ya mshambuliaji Meddie Kagere ambaye kwa siku za karibuni amekosa nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza cha kocha Sven.

Ziliibuka ripoti siku moja baada ya Simba kutwaa ubingwa wa ngao ya jamii ilipoifunga Namungo,kuwa Kagere na Sven walipigana mazoezini jambo ambalo lilikanushwa baadae.