Alhamisi , 8th Jan , 2015

Wananchi wa kijiji cha Nduoni kata ya Kirua Vunjo Magharibi mkoani Kilimanjaro wamefunga ofisi ya kijiji na kumpiga afisa mtendaji wa kata hiyo kwa madai ya kuchakachua matokeo ya uchaguzi uliopita.

Wananchi wa kijiji cha Nduoni kata ya Kirua Vunjo magharibi mkoani Kilimanjaro wamefunga ofisi ya kijiji na kumpiga afisa mtendaji wa kata hiyo kwa madai ya kuchakachua matokeo ya uchaguzi uliopita kwa kumtangaza mgombea wa Chama Cha Mapinduzi kuwa mshindi badala ya mgombea wa chama cha NCCR Mageuzi.

Wananchi hao walikusanyika katika ofisi ya kijiji hicho wakiwa na mabango mbalimbali na kusema kuwa wanasikitishwa na hatua ya serikali kumwapisha mgombea wa Chama Cha Mapinduzi Bw. Joseph Msaki aliyepata kura 158 na kumwacha mgombea wa chama cha NCCR mageuzi Bw. Thomas Ngowi aliyechaguliwa na wananchi kwa kupata kura 163.

Wamesema wamefikia hatua ya kufunga ofisi hiyo kwa madai ya kupewa kiongozi ambaye siyo chaguo la wananchi kwa kuwa serikali ilimwapisha kwa nguvu mgombea wa chama cha mapinduzi kuwa mwenyekiti wa kijiji hicho.

Kufuatia vurugu za wananchi hao afisa mtendaji wa kata ya Kirua Vunjo Magharibi Reginald Mlay alilazimika kumtangaza rasmi Bw. Thomas kupitia tiketi ya Chama cha NCCR Mageuzi kuwa ndiye mshindi halali wa kijiji hicho baada ya kupata kura 163 akifuatiwa na mgombea wa Chama Cha Mapinduzi aliyepata kura 158 na TLP kura Tisa

Naye mjumbe wa halmashauri kuu ya chama cha NCCR Mageuzi taifa Bw. Hemed Msabaha amesema mtendaji huyo alikiuka kanuni za uchaguzi kwa kuhujumu maamuzi ya wapiga kura jambo ambalo limesababisha vurugu ambazo zinatishia usalama.