Ijumaa , 20th Jun , 2014

Wajasiriamali wa kati wanaofanya biashara zinazotokana na mazao ya kilimo, Mifugo, na bidhaa za baharini kama Samaki na zile za misitu sasa watanufaika na fursa za kifedha sambamba na kupata ushauri na kujengewa uwezo wa namna ya kuboresha biashara.

Mwenyekiti wa taasisi ya sekta binafsi nchini Tanzania Dkt Reginald Mengi.

Akizindua asasi ya Kifedha jijini Dar es salaam inayojulikana kama Match Maker Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini Tanzania TPSF Dk. Reginald Mengi amesema kupitia asasi hiyo vijana wajasiriamali wa kati wataweza kukuza ajira mara baada ya kukuza biashara zao na hivyo kuwezesha kuleta amani na utulivu.

Dk. Mengi ambaye pia ni mwenyekiti mtendaji wa makampuni ya IPP pia amewashauri vijana wanaopata fedha hizo kwa kutumia mikopo yenye masharti nafuu kuhakikisha wanatimiza ndoto zao na kutokata tamaa kutokana na changamoto ambazo watakutana nazo katika biashara zao.

Kwa upande wake Mtendaji mkuu wa asasi hiyo ya Match Maker Bw. Edmond Ringo amesema asasi hiyo itawasaidia kupata fedha kwa masharti nafuu kutokana na wajasiriamali wengi wa kati kushindwa kupata fedha katika taasisi kubwa za fedha baada ya kushindwa kutimiza masharti.