Jumatatu , 30th Jan , 2023

Mkuu wa mkoa wa Kagera Albert Chalamila, amemtaka Kamanda wa Polisi mkoani humo William Mwampaghale, kuwaweka ndani wazazi wote watakaofika katika kituo cha polisi, kutoa taarifa za kupotea kwa watoto ili wafanyiwe uchunguzi kwanza kubaini kama kweli mtoto amepotea au kuna sababu nyingine

Mkuu wa mkoa wa Kagera Albert Chalamila

Akizungumza wakati wa kuapisha wakuu wa wilaya watatu kati ya watano walioteuliwa na wengine kuhamishiwa katika wilaya tano za mkoa wa Kagera, Chalamila amesema kuwa baada ya serikali kutangaza kusaka watoto ambao hawajaripoti shule, amegundua kuwa kuna mchezo unachezwa na wazazi, ambao wanafika katika vituo vya polisi na kuripoti kuwa watoto wao wamepotea, kumbe  baadhi yao wameozeshwa na wengine wapo wanatumikishwa.

"Sasa mzazi atakayekwenda polisi kutoa taarifa ya kupotea kwa mtoto akiomba kupewa RB kwanza akamatwe na kuwekwa ndani, na baada ya hapo afuatiliwe Mwenyekiti wa eneo husika naye akamatwe, wote hawa watoe ushirikiano kwa polisi na uchunguzi ufanyike ili kujiridhisha kama mtoto anayedaiwa kupotea kapotea kweli au ni uongo" amesema Chalamila.

Kuhusu wakuu wa wilaya walioteuliwa kushika wadhiwa huo katika Mkoa wa Kagera, Chalamila amewataka kutokukubali kuwekwa mfukoni, na badala yake washughulikie changamoto zinazokabili wilaya zao, ikiwamo migogoro ya ardhi, wizi wa mifugo, uingizaji wa raia wa kigeni, wizi wa kahawa, utoroshaji wa watoto kwenda mijini na uvuvi haramu.