Jumatatu , 18th Jan , 2016

Mwakilishi mkazi wa kampuni ya Dangote nchini ,Esther Baruti, ameomba radhi kufuatia taarifa zilizoandikwa kwenye vyombo vya habari wiki moja iliyopita juu ya kubainika kwa raia wa kigeni kiwandani hapo wanaofanya kazi bila kuwa na vibali.

Alhaji Aliko Dangote (kulia) mfanyabiashara maarufu kutoka Nigeria, akilakiwa na Mwakilishi Mkazi wa kampuni hiyo nchini, Esther Barut

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Mtwara mbele ya mkurugenzi wa sekta binafsi nchini (TPSF), Godfrey Simbeye, amesema majukumu aliyonayo ni kuhakikisha kampuni hiyo inatekeleza wajibu wake na kufuata taratibu zote za nchi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wafanyakazi wake wanakuwa na vibali.

Kwa upande wake, mkurugenzi wa sekta binafsi nchini, Godfrey Simbeye, amesema wafanyakazi raia wakigeni waliosimamishwa kuendelea na kazi kiwandani hapo kutokana na kukosa vibali, bado wapo nchini na kwamba serikali inalishughulikia suala lao ili kuhakikisha wale wanaokidhi vigezo vya kuendelea kufanya kazi warudi kazini.

Aidha, amesema alipata nafasi ya kukutana na meneja wa kiwanda hicho ambaye alikamatwa na maafisa wa Idara ya Uhamiaji kutokana na kutowapa ushirikiano walipokwenda kiwandani hapo, na alieleza masikitiko yake juu ya tukio hilo huku akiamini kuwa serikali inashughulikia suala hilo.