Vitanda vya shule ya Sekondari ya wasiochana ya Uchira Islamic viliungua kwa moto
Akizungumza kwenye kipindi cha SupaBreakfast cha East Africa Radio, hii leo Oktoba 17, 2020, Inspekta Abraham Ntezidyo, kutoka Jeshi la Zimamoto mkoa wa Kilimanjaro, amesema kuwa taarifa za moto huo walizipata jana jioni majira ya saa 12:00 na moto umeteketeza jumla ya vitanda 25 ambavyo walikuwa wakilala wanafunzi 50.
"Athari kubwa ni kwenye vitu vya wanafunzi na vitanda, wanafunzi hawakuwepo bwenini walikuwa wameenda Msikitini kwa ajili ya swala ya jioni, mpaka sasa hivi tunaendelea na uchunguzi wa moto huo ili kubaini chanzo na moto ulipoanzia", amesema Inspekta Abraham.
Aidha Inspekta Abraham ameongeza kuwa, "Hapa wanafunzi wako katika hali ya mshtuko, mikakati iliyopo tunakagua shule moja baada ya nyingine kwa kushirikiana na vyombo vingine na hata hii iliyoungua tunavyozungumza imekaguliwa juzi tu hata wiki haijaisha, lakini bahati mbaya imeungua, vyanzo vya moto viko vingi kuna umeme, hujuma, kuna vingine vinasababishwa kwa makusudi".