Jumatatu , 25th Apr , 2016

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora nchini Tanzania imesema asilimia 65 ya malalamiko kutoka kwa wananchi dhidi ya Jeshi la Polisi yanahusu ukiukwaji wa haki za msingi za watuhumiwa pamoja na kucheleweshwa kwa upelelezi wa kesi zinazowakabili.

Mtuhumiwa akifikishwa Mahakamani chini ya Ulinzi wa Polisi

Hayo yamebainika hii leo jijini Dar es Salaam wakati Tume hiyo ikiungana na nchi nyingine Barani Afrika kuadhimisha siku ya Afrika ya kuzinduliwa muongozo wa Luanda kuhusu haki za watuhumiwa wa makosa ya jinai, wanapokamatwa na kuzuiliwa mahabusu kabla ya kufunguliwa mashtaka.

Muongozo wa Luanda ulizinduliwa rasmi na Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu Mei 22,2014 huko Luanda nchini Angola ili kudumisha, kulinda na kukuza haki za raia katika mchakato wa haki jinai.

Dkt. Mandopi amesema kutokana na tafti zilizofanyika barani Afrika,ikiwemo Tanzania imebainika kuwa kuna uvunjifu mkubwa wa Haki za Binadamu kwenye mfumo mzima wa haki jinai ikiwa ni pamoja na watuhumiwa kupigwa, kuteswa, kubambikiwa kesi kunyimwa dhamana, kutofikishwa mahakamani watuhumiwa kwa wakati na kucheleweshwa kwa upelelezi.

Akizungumzia hali ya Magereza nchini Tanzania,Mkurugenzi wa Sheria wa Tume hiyo ,Nabor Assey amesema hali ya Magereza nchini siyo ya kuridhisha kutokana na bado kuwa na msongamano mkubwa.

Kwa Upande wake, Mwakilishi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Kaleb Lameck Gamaya amesema bado kumekuwa na ushinikizaji mkubwa wakati wa kuwakamata watuhumiwa licha ya kutii kukamtwa kwao ingawaje sheria inampa mamlaka askari kujiridhisha kama mtuhumiwa afungwe pingu ama la.

Tume hiyo inapendekeza kutumika vifungo mbadala ili kuondokana na msongamano uliopo magerezani.