Alhamisi , 3rd Mar , 2016

Ugonjwa kipindupindu umezuka tena katika mkoa wa Dodoma ambapo zaidi ya wagonjwa 27 wamegundulika katika kipindi kifupi tangu kuzuka kwa ugonjwa huo mwishoni mwa mwezi wa Februari.

Kaimu Mganga mkuu wa mkoa wa Dodoma , Dk, Nassoro Mzee(Kulia) akiwa na Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu

Akizungumza na East Africa Radio Kaimu Mganga mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk, Nassoro Mzee amesema tangu kuzuka kwa ugonjwa huo wilaya ya Kondoa pekee imegundulika kuwa na jumla ya wagonjwa 27.

Amesema tangu kuzuka kwa ugonjwa huo Agost mwaka jana Wilaya ya Kondoa ilikuwa haijawahi kuripotiwa kwa mgonjwa wa kipindupindu lakini ugonjwa huo umezuka na mmoja kati ya hao ameripotiwa kufariki dunia.

Amesema kutokana na hali hiyo juhudi mbalimbali zimekuwa zikichukuliwa ikiwemo kutoa elimu juu ya kuudhibiti ugonjwa huo, kubaini chanzo cha kutokea kwa milipuko hiyo ambapo kwa kushirikiana na wizara ya maji wamekuwa wakiyapima maji yanayotumiwa na wananchi na kubaini kama baadhi ya visima vinavyotumiwa na wananchi vina vimelea vya ugomnjwa huo.

Amebainisha kuwa mpaka jana wagonjwa walioripotiwa kuwa na kipindupindu ni 25 ambapo wilaya ya Mpwapwa ikiwa na wagonjwa wane, Manispaa kumi na Kondoa wagonjwa 11.

Daktari huyo amesisitiza kuwa kipindupindu katika mkoa wa Dodoma bado kipo na kutoa wito kwa wananchi kuzingatia kanuni za afya kwa kuzingatia suala la kuchemsha maji kabla ya kunywa, kunawa mikono kabla na baada ya kula, kunawa mikono watokapo chooni, kutojisaidia vichakani na kuzingatia matumizi ya vyoo bora na kusimamia sheria ndogo ndogo zilizopo.