Jumapili , 7th Dec , 2014

Watu wawili kati ya wanne wanaosadikiwa kuwa majambazi wameuawa na wananchi wenye hasira baada ya jaribio lao la kutaka kupora fedha zaidi ya shilingi milioni 100.

Watu wawili kati ya wanne wanaosadikiwa kuwa majambazi wameuawa na wananchi wenye hasira baada ya jaribio lao la kutaka kupora fedha zaidi ya shilingi milioni 100 katika kiwanda cha kutengeneza chokaa cha Nelkanth kilichopo eneo la Amboni jijini Tanga kushindikana.

Kaimu kamanda wa polisi mkoani Tanga kamishina msaidizi wa polisi Juma Ndaki amewataja majambazi waliouawa kuwa ni Timoth Charles mkazi wa Mkwajuni jijini Dar es Salaam na mwinyimkuu Hamisi mkazi wa mtaa wa chanika ambao walikuwa wakitumia usafiri wa pikipiki aina ya boxer huku wenzao wawili wakikimbia kusikojulikana.

Wakielezea vyema tukio hilo baadhi ya wafanyakazi na walinzi wa kiwanda hicho wamesema majambazi hao baada ya kuingia ndani ya geti la kiwanda hicho walikwenda moja kwa moja katika chumba cha mhasibu na walipofika walianza kunyonga mhasibu lakini wakati wa kujitetea ndipo sekretari wa mhasibu alipotoka nje na kupiga mayowe kuashiria bosi wake amevamiwa na majambazi.

Kufuatia hatua hiyo mmoja kati ya wafanyakazi wa kiwanda hicho Bwana Amiry Ramadhani ameliomba jeshi la polisi mkoani Tanga kuhakikisha wanafanya upelelezi wa kutosha ili kujua kama huenda kuna baadhi ya wafanyakazi ambao wamekuwa chanzo cha tukio hilo.