Jumapili , 7th Sep , 2014

Askari polisi 2 wameuawa na wengine 2 wamejeruhiwa na watu wanaodhaniwa majambazi waliovamia kituo cha Polisi Bukombe , Geita

Watu wanaosadikika kuwa ni majambazi wamevamia kituo cha polisi wilaya ya Bukombe na kuua askali polisi wawili na kujeruhi askali wengine wawili.

Akizungumza na waandishi wa habari, mkuu wa jeshi la polisi Igp Ernest Mangu amesema majambazi hao walivamia kituoni hapo saa Nane usiku ambapo walirusha mabomu na kuua askali wawili, waliouawa ni WP 7106 Uria Mwandiga na G 2615 Dastani Kimati waliojeruhiwa ni H627 Mohamed Hassan na CPL 5131 David Ngupama.

IGP Mangu amesema katika uvamizi huo silaha mbalimbali zimeibiwa ambapo jeshi la polisi limetangaza zawadi ya shilingi millioni kumi kwa yeyote atakayefanikisha kukamatwa kwa wahalifu hao na silaha zilizoibiwa.

Akithibitisha kupokelewa kwa majeruhi na miili ya marehemu mganga mkuu wa hospitali ya wilaya ya Bukombe daktari Honaratha Rutatinisibwa amesema hali za majeruhi ni mbaya na wamehamishiwa katika hospitali ya rufaa Bugando.