Alhamisi , 6th Oct , 2022

Helena Mashaka (13), mwanafunzi wa darasa la saba shule ya Shahende iliyopo Kata ya Butobela, mkoani Geita, amechomwa mikono yake kwa moto na Mama yake kwa tuhuma za kuiba shilingi 30,000 na kupelekea mwanafunzi huyo kushindwa kufanya mitihani yake ya kuhitimu.

Helena aliyechomwa moto mikono yake

Akizungumza kwa njia ya simu, Mtendaji wa Kijiji hicho Edgar Michael, amesema alipata taarifa ya mtoto huyo kujeruhiwa kutoka kwa mwalimu mkuu wa shule hiyo majira ya saa 2:00 asubuhi akidai kuwa kuna binti amechomwa moto na Mama yake na ameshindwa kufanya mitihani.

Baada ya kupata  taarifa hiyo wakamfuatilia mzazi kisha wakamkamata na kudai alifanya tukio hilo kwa sababu mtoto huyo aliiba shilingi 30,000 

Mpaka sasa mzazi huyo anashikiliwa na Jeshi la Polisi katika kituo kidogo cha Polisi kilichopo Kata ya Bukoli, na mwanafunzi amepelekwa Zahanati ya Bukoli kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

Aidha Mtendaji huyo amesema taratibu zinaendelea ili mwanafunzi huyo aweze kupata nafasi ya kurudia kufanya mitihani hiyo ya kuhitimu kwa mwaka 2023.